Hatutaogopa vitisho
KWA mara nyingine, tumeendelea kupokea vitisho kutoka kwa watu tusiowafahamu, nia yao ikiwa ni kutuogopesha ili tuachane na utoaji taarifa kuhusu mafisadi.
Vitisho hivi havikuanza leo, ni muendelezo wa juhudi za mfa maji anayetapatapa. Mapema mwaka huu, baada ya kupokea vitisho kama hivi, watu hawa waliajiri wavamizi ambao waliendesha shambulio kwa Mkurugenzi Mtendaji Saed Kubenea na mshauri wa gazeti Ndimara Tegambwage.
Nia ya uvamizi haikuwa kudhuru mwili tu, bali walitaka roho za wenzetu hawa. Kwa habati mbaya kwao nia yao haikutimia, sasa wameanza tena vitisho.
Tunaomba kuwaeleza wasomaji wetu kwamba sisi hatuogopi vitisho hivi. Tunaendelea kuandika. Kuandika ndiyo kazi yetu tunayopenda, tuliyochagua na tuliyosomea.
Tunachukua fursa hii kuwashitaki kwa umma, wale walioshiriki uvamizi na wote wanaotoa vitisho kwa shabaha ya kutunyamazisha. Tuacheni tufanye kazi yetu.
Hatukusudii kumwonea mtu, wala hatutajiruhusu kutumiwa na watu kuendeleza visasi kwa nia ya kukomoana. Tutasimama katika maadili ya uandishi wa habari kwa kusema kweli daima.
Tusichotaka kufanya na ambacho hatutaki kushurutishwa kufanya, ni kuwa sehemu ya mtandao wa kufunika wahalifu, kusafisha maovu ya watu au kuwabeba watu wachafu mbele ya jamii.
Tutatoa habari na taarifa. Wananchi wenyewe, ambao ni waajiri wetu, watasoma na kuchukua msimamo kadri watakavyoelewa. Huo ndio uandishi tuliokuwa tukifanya; tunaofanya hivi sasa na tunaokusudia kuendelea kufanya. Tuwe pamoja.
- Login or register to post comments
- Login or register to post comments
- Login or register to post comments