Sitta amtikisa Kikwete


Saed Kubenea's picture

Na Saed Kubenea - Imechapwa 17 November 2010

Printer-friendly versionSend to friend
Aliyekuwa spika wa Bunge la Jamhuri, Samwel Sitta

HATUA ya kumuengua aliyekuwa spika wa Bunge la Jamhuri, Samwel Sitta kwenye kinyang’anyiro cha uspika, ililenga kusafishia njia aliyekuwa waziri mkuu, Edward Lowassa, MwanaHALISI limeelezwa.

Taarifa kutoka ndani ya kikao cha Kamati Kuu (CC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilichofikia uamuzi wa kumuengua Sitta, zinasema mpango huo ulisukwa na kutekelezwa kwa ustadi mkubwa na mbunge wa Igunga, Rostam Aziz.

Lowassa anayekabiliwa na lundo la tuhuma za ufisadi anatafuta kila upenyo kuhakikisha anapata nafasi ya kushika utawala mwaka 2015.

Mjumbe mmoja wa CC aliyekuwa katika kikao kilichomuengua Sitta, na hakupenda kutajwa gazetini, amesema mkakati huo uliandaliwa na kutekelezwa na viongozi waandamizi ndani ya chama hicho.

Aliwataja viongozi hao kuwa Rostam Aziz, Edward Lowassa, Andrew Chenge na Yusuf Makamba ambaye ni katibu mkuu wa chama hicho. 

Kilichofanyika ndani ya kikao kilikuwa mwendelezo wa kile ambacho Chenge alifanya siku chache kabla ya uchaguzi wa spika.

Mjumbe huyo wa kamati kuu aliitisha mkutano wa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam na kutumia muda mwingi kumlaumu, kumlaani, kumshutumu na kumtuhumu Sitta kwa kile alichoita kuleta mgawanyiko katika chama na kudharalilisha serikali wakati akiwa spika (2005 – 2010).

Gazeti hili limefahamishwa kuwa aliyekuwa wa kwanza kushambulia Sitta alikuwa Haji Omari Kheri, mjumbe wa CC kutoka Zanzibar.

Kheri amenukuliwa na mtoa taarifa akimtuhumu Sitta kuwa ni mbinafsi na anayeendesha Bunge kibabe.

Mjadala juu ya Sitta uliibuka baada ya sektarieti ya chama hicho kupeleka katika mkutano wa CC majina matatu ya wagombea nafasi hiyo. Wagombea ambao majina yao yalipelekwa CC, ni Sitta, Anna Makinda na Anna Abdallah. 

Ni katika kujadili majina hayo matatu, ndipo Kheri aliibuka. Akiwa mzungumzaji wa kwanza katika kikao hicho, Kheri alisema, “Bwana huyu amejaa ubinafsi.”

Akiongea kwa ukali na msisitizo ambao haujulikani chanzo chake kwa kuwa Kheri hajawahi kuwa mbunge, wala kufanya kazi na Sitta bungeni alisisitiza, “Mwenyekiti, Sitta hatufai… Ni mbinafsi na amejaa ubinafsi.” 

Kauli ya Kheri iliungwa mkono na Spika wa Baraza la wawakilishi la Zanzibar, Pandu Ameir Kificho ambaye alimtuhumu Sitta kuwa ameligawa bunge na chama chake.

Kificho amenukuliwa akisema “mwenzetu” ameendesha bunge vibaya. Hakuleta umoja wala hakusimamia maslahi ya chama na kwamba Sitta ameleta madhara makubwa katika chama na bunge.

Taarifa zinaeleza alikuwa ni mwenyekiti wa kamati ya kampeni ya CCM, Abdulrahaman Kinana aliyetaka wajumbe kuachana na porojo kwamba Sitta amevuruga bunge. Alipendekeza Sitta aruhusiwe kutetea kiti chake.

Alisema, “Ukweli unabaki palepale, kwamba Samwel Sitta amelijengea heshima Bunge, chama chetu na yeye binafsi. Ametupa sisi na chama chetu heshima ya hali ya juu sana.”

Alisema, “Kama tunataka kumpa (uspika) mwanamke basi tumpe. Lakini bado nasisitiza, kwamba Samwel amefanya kazi na ametujengea heshima, na mimi binafsi sioni sababu ya kumuengua,” amenukuliwa Kinana akisema.

Lakini kauli ya Kinana ilizimwa mara moja na sauti ya Makamba iliyonukuliwa ikisema, “…naona huyu Kinana anamsifia sana Sitta. Kwani yeye hana kasoro?”

Akiongea kwa sauti ya juu, Makamba alisema, “…mbona Kinana hasemi mabaya ya Sitta? Kwani hana kasoro? Ndiyo tukubaliane basi kuwa Sitta anaweza kuwa na sifa, lakini kasoro zake mbona hazisemwi,” alihoji Makamba.

Naye Sophia Simba, kama ilivyokuwa kwa wajumbe waliotangulia, Kificho na Kheri, aliibuka na lundo la shutuma dhidi ya Sitta. Alisema kiongozi huyo alikuwa ameligeuza bunge kuwa kama chombo chake binafsi.

“Sitta ametugawa bungeni. Anajigamba na kujisifia. Kumpitisha tena kuwania nafasi hii, ni kujitafutia matatizo zaidi,” alinukuliwa Simba akisema.

Mara baada ya kumaliza kumshambulia Sitta, ndipo Simba akapendekeza kuwa CC ipitishe wagombea wanawake ili kuwezesha nafasi hiyo kushikiliwa kwa mara ya kwanza na mwanamke.

Hata hivyo, msimamo wa Simba ulipingwa na baadhi ya wajumbe kama vile, Kinana, Benard Membe na John Malecela. Viongozi hao waliendelea kusisitiza kuwa ni muhimu Sitta kupewa fursa ya kutetea nafasi yake.

Mjumbe mwingine aliyemtetea Sitta ni mkurugenzi wa Sera, Habari na Uenezi wa CCM, John Chiligati. Hoja ya kuwekwa spika mwanamke iliungwa mkono na viongozi wakuu wa nchi, akiwamo Rais Kikwete na rais mstaafu Ali Hassani Mwinyi.

Akiongea kwa sauti ya upole na iliyojaa diplomasia, Membe alinukuliwa akisema, “Chama chetu kiko hatarini iwapo baadhi ya viongozi wataendelea na utaratibu huu wa kung’ang’ania siasa za visasi, majungu na fitina.”

Alisema, “Kabla ya kufikia uamuzi huu, tumejiuliza kilichosababisha kutuangusha kutoka asilimia 80 mwaka 2005 hadi asilimia 61 mwaka 2010? Mbona tunajitengenezea bomu litakalotulipukia wenyewe?”

Mjumbe huyo alinukuliwa akisema Sitta ni miongoni mwa viongozi wachache sana ndani ya CCM ambao wanaheshimika mbele ya wananchi kutokana na msimamo wake wa kupinga vita vya ufisadi hadharani.

“Sitta amejijengea heshima kubwa ndani na nje ya bunge. Amekuwa akijitambulisha kuwa mpiganaji wa vita dhidi ya ufisadi. Sasa tukimuondoa kwa njia hii, nani ataelewa kwamba tumemuondoa ili kuweka spika mwanamke,” alihoji Membe.

Alisema kama lengo lilikuwa kuwa na spika mwanamke, hilo lingeelezwa mapema ili kutoa nafasi kwa Sitta kuachana na mpango wake wa kugombea nafasi hiyo.

Alisema kama walitaka kuweka spika mwanamke, “kwa nini hatukumshirikisha? Mbona hatukumueleza ili asaidie katika mchakato wa kumtafuta?”

Alisema iwapo angeshirikishwa angejiona kuwa ni sehemu ya mpango huo, kuliko hatua iliyochukuliwa ambayo “wengi wanaiona kama imelenga kumdhalilisha.”

Naye Chiligati aliweka msisitizo kuwa siasa za visasi na kukamiana haziwezi kukiweka mahali salama chama chao.

Wakati hayo yakitokea ndani ya mkutano wa CC, habari nyingine zinaeleza kuwa ni Rostam aliyesafiri hadi Iringa kukutana na Makinda ili kumshawishi kugombea nafasi ya spika.

Kabla ya kwenda Iringa, Rostam alikutana na Makinda kabla bunge la tisa la bajeti kufungwa.

Makinda amethibitishia mmoja wa marafiki zake wa karibu, ambaye ni mbunge, kwamba ni kweli aliombwa na Rostam kugombea nafasi hiyo.

Hata hivyo, alisema hiyo haina maana kwamba “…nimewekwa kulinda maslahi ya Rostam.”

“Hawa waliona kuwa ninaweza kumuangusha Sitta. Ndiyo wakanitafuta na kutaka kutumia fursa hiyo kumuangusha mbaya wao. Hii haina maana kwamba mimi nimewekwa nao,” Makinda amenukuliwa akieleza mwandani wake huyo siku moja baada ya kupitishwa na chama chake kuwania nafasi hiyo.

MwanaHALISI liliwahi kuchapisha taarifa kwamba kujitosa kwa Makinda katika nafasi hiyo kulitokana na kutekeleza ombi la Rostam.

Mara baada ya mpango wa kummaliza Sitta kufanikiwa, taarifa zinasema Rais Kikwete alituma ujumbe ili kuonana na Sitta. Waliotumwa na Kikwete wametajwa kuwa Malecela na Membe.

“Nimekutana na Sitta, lakini amesema hataki nafasi yoyote. Amepanga kuondoka katika chama kwa sababu familia yake na wenzake wengine wamemueleza kuwa hatakiwi katika chama,” kilisema chanzo cha taarifa kikinukuu mmoja wa wabunge ambao wanatajwa kuwa ni wafuasi wa Sitta. Haijafahamika kama Sitta anaendelea na msimamo wake huo.

Mbunge huyo aliongea na Sitta siku moja baada ya kiongozi huyo kuenguliwa kwenye kinyang’anyiro cha nafasi ya uspika.

Katika mazungumzo yake na rais ambayo yalidumu kwa saa nzima, tangu saa tatu asubuhi ya Alhamisi iliyopita, Sitta alieleza jinsi alivyodhalilishwa na uamuzi wa kumuondoa katika mbio za kutetea kiti chake, taarifa zimeeleza.

0
Your rating: None Average: 4 (6 votes)
Soma zaidi kuhusu:

Tanzania nchi yetu kweli nakuhurumia kuna watu ama mafisadi wanataka kuidumbukiza ktk janga kubwa na wimbi la damu nasema tema mungu tusaidie na uwakashifu hawa watu nakuwafikisha ktk mkondo wa sheria Aamin.

hii nchi haiwezi kwenda mbele kwa watu kuangalia maslahi yao na ya chama na si ya watanzania walio wengi.Tumeiuza nchi kwa kofia na tisheti zenye sura mbaya ya kiwete

hii nchi haiwezi kwenda mbele kwa watu kuangalia maslahi yao na ya chama na si ya watanzania walio wengi.Tumeiuza nchi kwa kofia na tisheti zenye sura mbaya ya kiwete

haswa huo ndio ukweli ambao haupingiki kwamba tanzania rais wake ni A.R. na si kiwete.

hizi nyingine ni exagration tuu sidhani kuwa kilichofanyika ni dhalala bali ni mageuzi tuu ya kawaida ambayo kila mtu anatakiwa kuyakubali. hebu tuone sasa ni jinsi gani haya mageuzi yatafanya kazi.Mzee sitta atabaki na heshima yake vile vile na natumaini kuwa ataendelea kuitumikia nchi yake vizuri kwa kuwa ni mtu anayejua maadili ya uongozi.

Kila lakheri CC na CCM.
Mbuyu wowote ardhini ulianza kwa mbegu ndogo na sifa ya kuitwa mbuyu ni ukubwa wake. Licha ya mbuyu kuitwa mbuyu bado mbuyu huu huu ukishakomaa haukui tena japo majani hujiyokeza ukweli hubaki palepale kuwa huanza kuoza kwa ndani. Mti huu aina ya mbuyu ukioza hutoa mbolea na mboleahiyo haitumiki na wanadamu bali mimea tegemezina hustawi vema kuliko muonekano wa mbuyu wenyewe.
Sita- Sita ni mtu aliyejiheshimu mno na kutenda mengi ya kiutawala ndani ya chama kwa nyadhifa yake ua uspika bila kuwa na upande. kwa asiyejua basi hakufatilia bali kalowea kuelezwa yaliyojiri.
Upinzani maana yake kubwa ni kuinoa chama tawala kwa kukosoa chochote kifanywacho na serikali iliopo kwa minajil ya kuendeleza maendeleo ya kitaifa.
kwa uongozi wa Sita tulipata kuwajua mafisadi na ufisadi wenyewe hadi kwa kutafsiriwa na yeyemwenyewe.
Je CCM walitaka wananchi tusijue kwa Sita kutokubali upinzani wayatoe maovu ya mafisadi ndipo aonekane mwema na akubalike nao?
Je nchi yetu kilasiku ni changa kwa mustakabali wa kipatochetu kitaifa kulinganisha na mikopo na misaada. Je ilikuwa ni kosa Sita kutilia mkazo ijadiliwe matumizi ya Richmond kupokea mabilioni wakati mabilioni hayohayo ndio tunayaomba kama misaada ya kufanyia maendeleao ya kitaifa?
Nisichoelewa ni je tulitaka Sita awe kama Kikwete kipindi cha uchaguzi kwakumnadi Mramba apigiwe kura kwa usafi aliomtakasa yeye kwa maslahi ya aitha apate kura ya urais wakati angali mchafu mbele ya wapigakura ndiposa akubaliwe? Lahasha.
Kila chenye mwanzo kina mwisho.
CCM ilitakiwa itumie busara kama alizokuwa nazo Sita dhidi yake. Wangelikuwa wema wasingekurupuka kwa kufanya uamuzi waliouchukua.
CCM ningependa muutazame msimamo wenu kisiaza zaidi kuliko kibinafsi. Kisiasa kuna pande mbili kuu.
1- Endapo huyu bwana Sita atamegeka toka CCM angalieni mgawanyiko utakuwa vipi. Mfano ni Mheshimiwa Shibuda, kutoka tu CCM imewagharimu kwakiasi gani? kifupi mmepoteza majibo manne kwa mgongo wake hata kama wannachi si wote waliomchagua awe mbuge upande wa CHADEMA. Picha hiyo hiyo muivishe kwa Mheshimiwa Sita. Je si kwamba sasa mtakuwa mmepoteza majibo mengine matano kama si manne na kuwa jumla ya majimbo nane au kumi mmeyapoteza? Suala ilikuwa si tu kumuengua bali ni jinsi gani pandezote mbili zitakuwa zimekubaliana au kujengeka japo mmoja wenu kaangushwa ili kulinda idadi ya wapigakura waliowapeleka huko.
2- Kwaupande wenu wenyewe wana CCM Je, ni wote watakuwa wameafiki kuenguliwa bila kuwaelimisha au kuwapa sababu za msingi?na je hakutatokea makundi miongoni mwenu wenyewe kwakuwa kuna pande mbili za wapenda haki wakiwa wapiganaji wa upisadi na wenye pesa zao yaani vyanzo vya mipasuko na waamuzi wakuu?
Mimi nilidahni ingekuwa vema kama CCM wangekuwa na disciplinary department ambayo kazi yake ni kunyoosha watu haswa wanaotetea ujinga na unyonyaji. Leo hii nimewafananisha na mbuyu hivyo kuoza ni wale wateteao mabaka ya uchafu ndani ya chama na mbuyu ukiwa chama chenyewe.
Kwahili lazima chama kitatakasika Ila kila lakheri CCM

Hiyo kamati kuu imemdhalilisha sana sitta,kitu ambacho sitta anatakiwa kikifanya ni kurudisha kadi ya uanachama na kuja chadema ili 2015 awe rais wa TZ.maana hao wa ccm hawana dhamira safi kama yake hivo ni ngumu sana kuelewana nao.

Huyo mama getruda Rwakatare ni mnafiki mkubwa anapotosha watu na hicho kikanisa chake kwa kusema kikwete ni chaguo la Mungu wakati uchaguzi umejawa na Utata dunia nzima inajua.Mimi nashauri waumini wanaosali kwa huyu mama waondoke maana anawatapeli bure.

Kuna kila sababu ya kupata Rais kutoka chama tofauti na CCM. Maana wananchi tunachagua Rais, lakini anayeongoza nchi ni mtu mwingine. Wakati sisi tujua kwamba Kikwete ndiye rais wetu, lakini uhalisia ni kwamba anayeongoza nchi ni Rostam Aziz. Hii ni hatari sana kwa taifa letu.

Makinda hafai kwakua hupendelea kuzima hoja nzito na anatazama maslahi ya chama badala ya maslahi ya taifa.Sitta amehujumiwa muda mrefu,wananchi wanamwamini kwa ukamanda wake,akihama ccm ataondoka na kundi kubwa na akigombea urais atapata.